Huduma ya ujumbe Whatsapp imetangaza kuwa itayalinda mawasiliano ya wateja wake kuanzia hapo siku ya Jumanne April 5,mwaka huu
Huku
ulinzi ukiwekwa mwanzo na mwisho wa ujumbe ,ujumbe hautaharibiwa wakati
unapotoka katika simu ya anayeutuma na unaweza kusomwa pekee na
anayeupokea.
Hatua hiyo itaufanya ujumbe huo kutosomeka iwapo mhalifu ama hata maafisa wa polisi wanajaribu kuingilia simu bila idhini.
WhatsApp ambayo ina wateja zaidi ya bilioni moja duniani imesema kuwa uhamisho wa faili pamoja na sauti pia zitalindwa.
Huduma hiyo inayomilikiwa na kampuni ya Facebook imesema kuwa ulinzi wa mawasiliano ya faragha ni miongoni mwa malengo yake.
Ulinzi
huo uliathiriwa wakati shirika la Marekani la FBI lilipotaka kampuni ya
Apple kuisadia kuchukua data katika simu moja ya iphone iliotumiwa na
muuaji Syed Farook.
Whatsapp ilisema:Wazo hilo ni rahisi,
unapotuma ujumbe mtu pekee anayeweza kuusoma ni mtu ama kundi la
mawasiliano ambalo umelitumia ujumbe huo.
Hakuna mtu anayeweza kuusoma ujumbe huo hata kama ni wahalifu wa mitandaoni ama hata serikali.hata sisi hatuwezi kuusoma.
Watumiaji wapya wa huduma hiyo waliarifiwa kuhusu mabadiliko hayo wakati wanapotuma ujumbe siku ya Jumanne ya April 5,mwaka huu
Utafiti uliofanywa mwaka jana na Kampuni ya Utengenezaji wa simu ya Nokia kabla haijabadilishwa na kuwa Microsoft kuhusu biashara ya mauzo ya simu katika nchi mbalimbali barani Afrika,Tanzania ikiwa ni miongoni mwao,umebaini kuwa kuna mianya ambayo imekuwa ikitumika kuingiza simu hizo kwa njia za magendo bila kulipia ushuru huku ukiikosesha Serikali ya Tanzania kiasi cha shilingi bilioni 91.23. Utafiti huo unaeleza kuwa njia ambazo zimekuwa zikitumika ni upitishaji wa simu katika maeneo ya pembezoni mwa nchi hususani mikoa iliyoko mipakani mwa Tanzania na nchi jirani na kuingiza simu za magendo kupitia katika viwanja vya ndege vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es salaam na ule wa Kilimanjaro ambapo wafanyabiashara hulipia kiasi kidogo cha fedha ambazo hukadiliwa bila kuangalia uzito na thamani ya mzigo alionao. Takwimu za utafiti huo zinaonesha kuwa kwa wastani,simu za kawaida takribani 750,000 huuzwa kwa mwezi nchini Tanzania ambapo wastani wa bei kwa simu moja ni Sh 35,000 ambapo jumla ya mauzo ni Sh bilioni 26.2,huku kwa upande wa simu za kisasa kwa mwezi zikiuzwa simu 87,000 na wastani wa bei ikiwa ni Sh 250,000 ambapo mauzo yake kwa mwezi ni sawa na Sh bilioni 21.75. Jumla ya simu zinazouzwa kwa mwezi ni 837,000 ambapo thamani yake ni Sh Bilioni 48,kama zimu zote zitalipiwa ushuru wa asilimia 18 na mianya yote kufungwa basi serikali inastahili kukusanya Sh.Bilioni 8.64 kwa mwezi.
Kikundi cha kihalifu mtandao cha #Anonymous kimetekeleza mashambulizi mtandao dhidi ya Nchi ya Angola na kufanikiwa kudukua na kuangusha Tovuti 20 za serikali ya Nchi Hiyo.
Hatua hiyo ya kikundi hicho imefuatia baada ya kushinikiza serikali ya
Nchi hiyo kuwaachia watu 17 waliokamatwa kutokana na uasi dhidi ya
Serikali ya Rais Jose Eduardo dos Santo. Tukio hilo la Mashambulizi limepokelewa kwa masikitikomakubwa na jumuia ya wana usalama mitandao huku usaidizi wa dhati kuimarisha usalama kwa tovuti za Nchi hiyo zikichukuliwa.
Matukio ya kushambulia Serikali za Nchi za Afrika kimtandao yamepata
kuonekana mara kadhaa ambapo Ghana pia ilipata kua muathirika.
Baada ya Serikali ya Tanzania kuanzisha kampeni ya kuondosha matumizi ya simu zisizohalisi toka Disemba mwaka jana,ambapo simu hizo hazitaendelea kutumika ifikapo Juni mwaka 2016 huku ikielezwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kuwa kuna asimilia 40 ya simu zinazotumika nchini humo ambazo ni halisi. TCRA na Makampuni ya Huduma za Mawasiliano ya Simu za Mkononi Tanzania kwa sasa wanaendesha kampeni ya kuhakiki simu ya mtumiaji kama ni halisi ama si halisi kwa kutumia IMEI ya simu kuituma kwenda namba 15090. Mtandao wa kijamii wa WhatsApp ulio na watumiaji bilioni moja duniani katika mawasilino miongoni mwao wakiwemo watanzania,nao hauko nyuma katika kutafuta kilichobora kwai umetangaza kuwa ifikapo Disemba 2016 hatutatumika katika baadhi ya simu zilizopo duniani.
Huduma ya WhatsApp haitatumika tena
katika simu zinazotumia mifumo kadha ya programu endeshi ikiwemo Blackberry 10,
Nokia Symbian S60 na Windows Phone 7.1.
Kampuni ya Facebook
inayomiliki huduma hiyo imesema inataka kuangazia kustawisha “huduma
katika mifumo inayotumiwa na watu wengi. Kampuni hiyo imejitetea na kusema kwamba haijawatupa wateja wake ambao
wamechangia sana katika ufanisi wake lakini ni kutokana na mabadiliko ya
teknolojia.
Orodha kamili ya mifumo ya simu ambayo wateja hawataweza tena kutumia WhatsApp ni hii hapa:
Android 2.1 and Android 2.2
Blackberry OS 7 and earlier
Blackberry 10
Nokia S40
Nokia Symbian S60
Windows Phone 7.1
Kampuni hiyo imesema wakati wa kuanzishwa kwa WhatsApp mwaka
2009, asilimia 70 ya simu wakati huo zilikuwa za BlackBerry na Nokia."
Lakini sasa asilimia 99.5 ya simu zinatumia mifumo ya Google, Apple na Microsoft. Chanzo:BBC
Meneja
Uhusiano wa kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Nicodemus Thomas Mushi
akizungumza na vyombo vya habari leo jijini Dar es Salaam kukanusha
taarifa za kampuni hiyo kudukuliwa.
Meneja
wa Kitengo cha Usalama Mifumo ya Mawasiliano ya TTCL, Lina Rujweka
akifafanua jambo kwenye mkutano na vyombo vya habari.
Kampuni ya Simu
Tanzania (TTCL) imekanusha taarifa zinazosambaa mitandaoni kuwa mfumo wa
mawasiliano wa kampuni hiyo umeingiliwa na wadukuzi. Taarifa iliyotolewa juma hili
kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam na Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo, Nicodemus
Thomas Mushi alisema taarifa zinazotolewa si za kweli hivyo kuwataka wateja wao
wazipuuze.
“Tunapenda kuwathibithia Wateja wetu wote
wa ndani na nje ya nchi, wadau wetu na Umma kwa ujumla kwamba, taarifa hizi si
sahihi, na kwamba mifumo yetu ya Mawasiliano ya TTCL ipo salama, huduma zetu
zote zipo thabiti na mpaka sasa tunapotoa taarifa hii, hakuna uhalifu wowote
uliofanyika kwa sisi wenyewe kama Kampuni wala kwa mteja wetu yeyote,” alisema Thomas
Mushi.
Aidha, tunapenda
kuwathibitishia kuwa, taarifa za Wateja wetu wote ikiwemo Serikali , Idara,
Wakala na Taasisi za Umma, Taasisi za fedha, Mashirika, Makampuni na Watu
binafsi zipo salama kabisa. Ukweli huu unathibitishwa na Wateja wao pia kwani
hadi sasa, hakuna hata mmoja aliyeleta taarifa za kukosa huduma ama kupata
athari zozote kutokana na tetesi hizo.
Hata hivyo, alisema
pamoja na taarifa hizo, Wataalamu wa kampuni hiyo wanaendelea kuwa macho kwa
muda wote, ili kuhakikisha kuwa, wanafanyia kazi kila taarifa ama tishio la
kiusalama linaloweza kujitokeza katika mfumo wao.
“TTCL inaendelea
kuwaomba Umma na Wateja wetu wote kuendelea na majukumu yao kama kawaida bila
wasiwasi wowote. TCCL inawaleta Karibu.” Alisema Thomas Mushi.
Kwa upande wake
Meneja wa Kitengo cha Usalama Mifumo ya Mawasiliano ya TTCL, Lina Rujweka
alisema kitengo chao baada ya tetesi hizo kimefanya uchunguzi wa kina na hakuna
ashirio lolote la mifumo yao kuingiliwa (kudukuliwa) kama ilivyoelezwa.
Alisema kitengo
hicho kina wataalam ambao muda wote wapo kazini kufuatilia ufanisi wa mfumo wa
mawasiliano wa kampuni yao hivyo kuwaondoa hofu wateja wao.
“Baada ya
taarifa hizo Kitengo cha Usalama wa Mifumo ya Mawasiliano ya Kampuni ya TTCL
kiliingia kazini ili kubaini ukweli wa taarifa hizo na kufanya majaribio ya
kitaalamu ili kuthibitisha usalama wa mifumo yetu. Baada ya utafiti wa kina na
majaribio ya kitaalamu, tunapenda kuwathibithia Wateja wetu wote wa ndani na nje
ya nchi, wadau wetu na Umma kwa ujumla kwamba, taarifa hizi si sahihi...”
alisema.
Mkuu wa Kitengo cha Vifaa vya Mawasiliano wa Tigo, David Zakaria akielezea athari za matumizi ya simu bandia kwa waandishi wa habari (Hawapo pichani) katika mkutano uliofanyika mapema leo katika makao makuu ya Tigo Kijitonyama Dar es salaam., kushoto kwake ni Meneja wa Mawasiliano, John Wanyancha
Watumiaji wa simu za mkononi wameonywa dhidi
ya matumizi ya simu bandia na zisisokidhi viwango vya ubora ambazo tayari
zimetangwa kupigwa marufuku na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuanzia
mwezi Juni mwaka huu.
Kutokana na sababu hiyo, Tigo, ambayo ni kampuni ya kidijitali,
imeanza kuendesha kampeni ya kuhamasisisha wateja wake na umma kwa jumla kupitia
vyombo vya Habari inayolenga kuwaepusha na athari za matumizi ya simu bandia.
Kwa mujibu wa maelekezo ya
TCRA matumizi ya simu za mkononi ambazo namba zake za utambulisho wa kimataifa
(IMEI) ni bandia yatapigwa marufuku kutumika kwa mitandao yote ya simu nchini
Tanzania kuanzia Juni 16 mwaka huu. Ili kujiepusha na usumbufu wowote
utakaotokana na hatua hii tunawashauri wateja wetu kujipatia simu halisi na
bora kutoka maduka ya Tigo yaliyo karibu nao,`` alisema Mkuu wa Kitengo cha Vifaa vya Mawasiliano wa Tigo, David Zakaria.
Ripoti ya utafiti ulichapishwa katika tovuti ya GSMA ("http://www.gsma.com" www.gsma.com ) inasema kwamba tofauti na ilivyo
kwa simu halali ambazo hupitia mamia ya hatua mbalimbali za kuhakiki ubora wake
kabla ya kupelekwa sokoni, simu bandia hazifanyiwi majaribio ya ubora na kuna taarifa
za kitafiti zinazoonyesha kuwa baadhi ya simu bandia zina kiwango kikubwa cha
madini ya risasi na vitu vingine ambavyo ni hatari kwa mazingira na afya ya
binadamu.
Ripoti hiyo inaendelea kusema kuwa simu feki zinatengenezwa na
malighafi dhaifu zisizokidhi viwango na zimeshaonesha kuwa kiwango cha hatari
cha vyuma na kemikali kama risasi hadi kufikia kiwango cha mara 40 zaidi kuliko
kiwango kilichoidhinishwa na sekta ya mawasiliano duniani kwa mujibu wa na
Jukwaa la Watengenezaji wa Simu za Mkononi (MMF).
Akizungumza kuhusu hatua ya Tigo kutoa tahadhari kwa wateja wake
Zakaria alisema, ``Wanunuzi wanatakiwa kuwa waangalifu wakati wanaponunua simu
mpya au vifaa vya mawasiliano madukani au katika intaneti kwa sababu bidhaa
nyingi feki zinatengenezwa kwa kuigaa muundo na nembo za kibiashara za bidhaa
halisi kwa makusudi ili kuwalaghai wateja.
``Ili kuweza kuelewa iwapo simu yako ni feki au ni halisi unatakiwa
kupiga namba namba *#06# ambapo atapokea
namba ya IMEI ya simu hiyo na kisha kutima kwa njia ya jumbe mfupi
kwenda namba 15090 ambapo utapata jibu iwapo simu hiyo ya mkononi ni halisi au
ni bandia,” alisema Zacharia.
Meneja Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania TCRA Innocent Mungy, akizungumza na waandishi wa habari Zanzibar kuhusiana na kutambua Simu Feki na kudhibiti uingiaji wa Simu hizo Tanzania na kueleza mwisho wa matumizi wa simu hizo Nchini Tanzania ni Juni 2016. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View Kilima Zanzibar na kuwashirikisha waandishi wa Vyombo mbali mbali vilioko Zanzibar.
Naibu Mkurugenzi Masuala ya Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano TCRA Thadayo Ringo, akizungumza na waandishi wa habari jinsi ya kutambua Simu feki wakati wa mkutano huo na waandishi wa habari Zanzibar uliofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View Kilimani Zanzibar, Amesema utambuzi wa kujua simu yako kama ni orijinali unaweza kupiga namba kuaza na Nyota Reli 06 Reli . *# 06# na utapata ujumbe wa Simu yako kwa Mfano zitakuja tarakimu 15 mfano IMEI 12456789067654 Na Kupiga 15090 Ujumbe wa kukuelewesha kama ni simu yako orijino. kwa mfano kama huu Sony Mobile Communications AB -SONY C5555 - Xperia. huu ni mfano wa kujua simu orijino.
Naibu Mkurugenzi Masuala ya Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano Thadayo Ringo akionesha mfano wa simu orijino kwa waandishi wa habari wakati wa mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View Kilimani Zanzibar.
Waandishi wa habari wakifuatilia mkutano huo wa TCRA uliofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Ocean View Kilimani Zanzibar. Imetayarishwa na Othman Mapara.Blogspot
Kampuni kubwa ya teknolojia ya
Apple imesema mauzo ya simu zake zijulikanazo kama iPhone yameanza
kupungua na kwamba mauzo hayo yanatarajiwa kushuka kwa mara ya kwanza
tangu kuzinduliwa kwa simu hizo 2007.
Kampuni hiyo kutoka Marekani
iliuza simu 74.8 milioni robo ya kwanza ya mwaka huu wa kifedha
ikilinganishwa na simu 74.5 milioni robo ya kwanza ya mwaka
uliotangulia. Apple imesema mauzo kutoka kwa robo ijayo yanatarajiwa
kuwa kati ya $50 bilioni na $53 bilioni, kiasi ambacho kitakuwa chini ya
mauzo ya $58 bilioni kipindi sawa mwaka uliotangulia.
Hii itakuwa mara ya kwanza kwa mauzo ya iPhone kushuka tangu kuzinduliwa kwa simu hizo za kisasa.
Mauzo ya iPhone yalichangia asilimia 68 ya faina ya kampuni ya Apple mwaka jana.
Kushuka kwa mauzo ya kampuni hiyo kunadaiwa kutokana na kiwango cha uchumi wa China kushuka.
Mauzo
ya Apple nchini China, Hong Kong na Taiwan yaliongezeka 14%, lakini
kiwango hicho cha ukuaji ni cha chini mno kikilinganishwa na ukuaji wa
70% ulioshuhudiwa mwaka mmoja uliopita.
Kampuni ya vifaa vya kielektroniki, Samsung imeathiriwa na kushuka kwa mauzo ya simu zake za aina ya Smartphone.
Mazingira
mabaya ya kibiashara na viwango vya chini vya vifaa vya kiteknolojia
vilisababisha kushuka kwa faida katika robo ya nne ya mwaka jana kwa
asilimia 40 hadi dola bilioni 2.7.
Kampuni hiyo ya Korea Kusini imeonya kwamba itakuwa vigumu kudhibiti faida mwaka huu kama ilivyokuwa mwaka 2015.
Mapato ya mwaka 2015 yalishuka hadi dola bilioni 165 ikilinganishwa na miezi 12 iliopita.
Ushindani
mkali kutoka kwa kampuni za Uchina zinazotengeza vifaa rahisi vya
kiteknolojia kama vile Xaiomi na Huwawei katika soko hilo pamoja na
kampuni ya Apple zimeathiri mauzo ya simu za Smartphone.
Simu ya Galaxy S6,ambayo ndio simu ya hadhi ya juu iliozinduliwa
mnamo mwezi Aprili,ilishindwa kuwafurahisha wateja na kampuni hiyo
imeshindwa kudhibiti soko lake.
Jake Saunders,mkurugenzi wa
Asia-Pacific katika kampuni ya utafiti ya ABI Research,ameiambia
BBC:''Inaonyesha kwamba wako chini ya shinikizo kwa sababu nusu ya
mapato yao yanatoka katika simu za rununu''.
Xiaomi inapata wateja
katika soko la India na Indonesia,ambalo ni kubwa kwa simu za
smartphone na ndio eneo ambalo linakuwa kwa haraka.
Kampuni ya usalama mtandaoni ya SplashData imetoa orodha ya nywila au maneno ya siri yaliyotumiwa sana na watu mwaka uliopita.
Orodha hiyo imetayarishwa kwa kutumia maneno ya siri zaidi ya milioni mbili yaliyofichuliwa na wadukuzi mwaka uliopita.
Mwaka
huu, neno ‘Star Wars’, kutoka kwa mwendelezo wa filamu za Star Wars,
lilikuwa miongoni mwa maneno 25 yaliyotumiwa zaidi. Filamu ya Star Wars:
The Force Awakens ilizinduliwa mwezi Desemba.
Wengi bado wanatumia ‘123456’ kama nywila na wengine ‘password’. Ili kuwa salama mtandaoni, huwa ni vyema kutumia nyila ambayo watu wengine hawawezi wakaifikiria au kugundua kwa urahisi.
Moja ya njia za kuimarisha neno la siri ni kuchanganya tarakimu, herufi na alama pamoja na kuchanganya herufi kubwa na ndogo.
Lakini wengi hutatizika katika kukumbuka nywila.
Moja ya njia unazoweza kutumia ni kuangalia maneno ya wimbo uupendao na kuyafupisha.
Hapa kuna mfano wa jinsi unaweza kupata nyila kutoka kwa wimbo.
Chagua mwanamuziki umpendaye, tuseme
Chagua wimbo wake
Tafuta mstari mmoja, sana ukupendezao zaidi,
Fupisha kwa kuchukua herufi ya kwanza
ya kila neno, au herufi mbili za kwanza. Tukichukua herufi mbili za
kwanza.
Changanya herufi kubwa na ndogo
Kisha, badilisha herufi zinazokaribiana na tarakimu kuwa tarakimu, mfano badala ya ‘a’ tumia ‘@’ na badala ya ‘i’ tumia ‘1’.
Ni vigumu mtu
kuigundua kwa urahisi lakini kila ukikumbuka wimbo wako unaweza
ukaikumbuka kwa urahisi.
Vifaa vya mawasiliano vya mkononi –
hususan simu za kiganjani na vifaa vya mawasiliano vya kiganjani (tablets) –
vina namba maalum inayovitambulisha. Namba hiyo inajulikana kama IMEI ambacho
ni kifupi cha International Mobile Equipment Identity.
Kifungu cha 84 cha Sheria ya
Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) ya 2010 kinataka kuwepo kwa mfumo
wa rajisi ya namba za utambulisho wa vifaa vya mawasiliano vya mkononi. Rajisi
hii inajulikana kwa kiingereza kama Central Equipment Identification Register,
kwa kifupi CEIR. Sheria inataka rajisi hiyo ihifadhiwe na kuendeshwa na Mamlaka
ya Mawasiliano Tanzania.
Aidha Kanuni za mwaka 2011 za EPOCA
kuhusu mfumo wa rajisi ya namba za utambulisho wa vifaa vya mawasiliano vya
mkononi inawataka watoa huduma wa mawasiliano yanayotumia vifaa vya mkononi
kuweka mfumo wa kudumu wa kumbukumbu za namba tambulishi (Equipment Identity
Register – EIR) za vifaa vya mkononi vinavyotumika kwenye mitandao yao.
Mfumo huu wa kielektroniki ambao
utahifadhi kumbukumbu za namba tambulishi za vifaa vya mawasiliano vya mkononi
una lengo la kufuatilia namba tambulishi za vifaa vinavyoibiwa, kuharibika,
kupotea au ambavyo havikidhi viwango vya matumizi katika soko la mawasiliano.
Vifaa vyote vya mawasiliano vya
mkononi ambavyo vimeibiwa, vimeharibika, kupotea au visivyokidhi viwango vya
matumizi katika soko la mawasiliano havitaweza kufanya kazi kwenye mitandao ya
mawasiliano kutumia vifaa vya mkononi.
UFAFANUZI
Taarifa kwenye mfumo huu wa rajisi zitakuwa na aina tatu za kumbukumbu; ambazo
ni orodha ya namba tambulishi ambazo vifaa vyake vinaruhusiwa, orodha ya namba
tambulishi ambazo zimetolewa taarifa kuwa zimefungiwa na namba tambulishi
ambazo zimefungiwa kwa muda au kuruhusiwa kwa muda.
Orodha Nyeupe:
Orodha ya vifaa vya mkononi vya mawasiliano vinavyoruhusiwa kutumika katika
mitandao ya huduma za simu za kiganjani
Orodha Nyeusi:
Orodha hii ni ya namba tambulishi ambazo zimefungiwa na mtoa huduma kwenye
mfumo wao wa EIR na kutumwa kwenye mfumo wa CEIR kwa ajili ya kufungiwa ili
zisitumike kwenye mitandao mingine ya simu za kiganjani kwa mujibu wa utaratibu
uliowekwa na kukubaliwa miongoni mwa watoa huduma. Simu zote za mkononi
zilizoibiwa au kupotea zitafungiwa ndani ya saa 24 ili zisitumike kwenye
mtandao wowote wa simu za mkononi Tanzania.
Ikitokea simu ya mtumiaji ikafungiwa
kinamosa, anatakiwa kutoa taarifa mara moja kwa mtoa huduma wako kwa ajili ya
kuifungua. Watoa huduma wanatakiwa wafungulie, ndani ya saa 24, simu zote
zilizofungwa kimakosa.
Orodha ya kijivu:
Orodha hii ni ya namba tambulishi ambazo zimefungiwa au kufunguliwa kwa muda
kwa lengo la kuanzisha mchakato wa kuzifuatilia.
FAIDA ZA MFUMO WA RAJISI YA NAMBA TAMBULISHI
Mfumo huu wa rajisi una faida zifuatazo:
1. Kuthibiti wizi wa simu. Iwapo mtu atapoteza au ameibiwa simu ya kiganjani na
akatoa taarifa kwa mtoa huduma, simu hiyo itafungiwa isiweze kutumika kwenye
mtandao mwingine wowote wa simu za kiganjani. Mteja anaponunua simu ni lazima
adai risiti halali na halisi na pia garantiii ya angalau miezi 12. Mteja
anatakiwa aihifadhi risiti hiyo angalau kwa miezi mitatu. Baada ya hapo, iwapo
simu imekuwa inatumika, taarifa za matumizi zinaweza kutumika kama uthibitisho
mbadala wa milki ya simu husika.
2. Kuhimiza utii wa sheria: Kifungu
cha 128 cha EPOCA kinamtaka mtumiaji wa simu kutoa taarifa ya kupotea au
kuibiwa kwa simu au laini ya simu. Kifungu cha 134 kinayataka makampuni ya simu
kutokutoa huduma kwa simu ambayo imefungiwa kama ilivyoelezwa hapo juu. Mara tu
mteja anapopoteza simu yake ya kiganjani anatakiwa kutoa taarifa kwa kituo cha
Polisi cha karibu ambapo atapewa namba ya kumbukumbu ya taarifa ya tukio,
maarufu kama RB.
Anatakiwa aende kwa mtoa huduma
kutoa taarifa ya tukio akiwa na hiyo RB na uthibitisho wa umilki wa simu
iliyopotea ( risiti aliyopewa wakati wa kununua iwapo itakuwepo). Mtoa huduma
kwanza atahakiki umilki wa simu iliyopotea au kuibiwa na atampatia mteja namba
ya kumbukumbu kwamba simu hiyo imefungiwa isutumike kwenye mitandao ya simu na
hatimaye ataifungia simu hiyo ndani ya saa 24.
3. Kujenga misingi ya matumizi ya
simu halisi, zisizo bandia. Mtumiaji ataweza kutambua iwapo simu aliyo nayo
inakidhi viwango, ni halisi na sio bandia.
KUTAMBUA NAMBA TAMBULISHI
Ili kutambua namba tambulishi ya simu ya kiganjani au vifaa vya mawasiliano ya
kiganjani, mtumiaji anatakiwa aandike tarakimu *#06# kwa kutumia kifaa chake.
Baada ya kufanya hivyo, kutaonekana namba ndefu. Mtumiaji anatakiwa kuandika
namba hiyo kama ilivyoonekana kwenye kifaa chakena kuihifadhi katika hali ya
usalama kwa ajili ya rejea ya baadae.
Baada ya hapo mtumiaji atume ujumbe
mfupi wenye hiyo namba tambulishi kwenda namba 15090. Atapokea meseji
itakayomjulisha kuhusu hali halisi ya simu yake ya kiganjani. Mtumiaji atapokea
ujumbe kuhusu uhalisia wa simu yake. Majibu yatakayokuja yatasomeka: Kama IMEI
haioani na aina ya simu yako, wasiliana na aliyekuuzia. Usipoweza,ibadilishe
kabla ya Juni 2016 kwani simu hiyo inaweza kuwa BANDIA.
HATUA ZA KUCHUKUA IWAPO SIMU
ITAONEKANA HAIKIDHI VIWANGO, SI HALISI NA NI BANDIA
Mtu yeyote ambaye atatambua kwamba
simu yake ya kiganjani si halisi,ni bandia na haikidhi viwango atapewa muda wa
kuendelea kutumia simu hiyo. Baada ya muda huo kumalizika, simu hiyo itaingizwa
katika orodha nyeusi na kufungiwa isitumike kwenye mitandao mingine yoyoye ya
simu za kiganjani.
Watumiaji wote wenye simu za
kiganjani ambazo namba tambulishi zao zinaonyesha kwamba simu hizo si halisi,
ni feki na hazikidhi viwango watagharamia ununuzi wa simu nyingine.
Watumiaji wote ambao namba
tambulishi za simu zao zinaonyesha kwamba vifaa hivyo si halisi, ni feki na
havikidhi viwango watatakiwa kubadilisha simu hizo na kupata zinazokidhi
viwango na halisi katika muda wa miezi sita kuanzia siku ya uzinduzi wa mfumo
wa rajisi ya namba za utambulisho wa simu za kiganjani.
Ni vyema ifahamike kwamba simu zote
za kiganjani na vifaa vya mawasiliano vya kiganjani (tablets) ambazo zitakuwa
na namba tambulishi bandia zitafungiwa kuanzia 16 Juni 2016.
HITIMISHO
Mfumo wa Rajisi ya Namba za Utambulisho wa vifaa vya mawasiliano vya mkononi
una lengo la kuwahakikishia watumiaji usalama wakati wanapotumia vifaa hivyo
vya mawasiliano, vikiwemo simu za kiganjani na vifaa vya mawasiliano vya
kiganjani (tablets). Uanzishwaji wake ni sehemu ya kutekeleza matakwa ya Sheria
ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta ya 2010. Ni vyema watumiaji
wakazingatia maelekezo kuhusu utaratibu wa kuhakiki namba tambulishi, kutoa
taarifa wanapopoteza au kuibiwa simu.
Imetolewa na:
Mkurugenzi Mkuu
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania
18 December 2015