Thursday, January 14, 2016

ASILIMIA 60 YA WAKAZI DUNIANI HAWANA NJIA YA KUTUMIA MTANDAO WA INTANETI



 


Wakaazi bilioni 4.2 wa dunia hawana njia ya kutumia mtandao wa Intaneti.
 
Idadi hiyo ni sawa na asili mia 60 ya wakaazi wa dunia-benki kuu ya dunia imesema hayo mjini Washington. 

Kumeibuka "pengo la digitali" kutokana na ule ukweli kwamba intanet inakutikana zaidi katika nchi tajiri. 

Nchini India watu bilioni moja nukta moja hawana mtandao wa intaneti,nchini China wanafikia watu milioni 755 na Indonesia watu milioni 213. 

Pengo hilo linazidi kuwa pana linapohusika suala la intaneti ya haraka-inasema benki kuu ya dunia. 

Wanaofaidika na  intaneti kama hiyo ni watu bilioni moja nukta moja tu-ikimaanisha chini ya asilimia 15 ya wakaazi jumla wa dunia.

"Watu wanabidi wajiepushe isiibuke "tabaka mpya ya wanaobaguliwa kijamii" anaonya mwanauchumi mkuu wa benki kuu ya dunia Kaushik Basu katika ripoti yake iliyopewa jina "Faida ya teknolojia ya habari."

AFRIKA KUSINI KUDHIBITI WHATSAPP NA VIBER

 

 
Mitandao ya whatsapp na viber huenda ikadhibitiwa Afrika Kusini ikitegemea matokeo ya vikao vya bunge baadaye mwezi huu, umeripoti mtandao unaoheshimika wa Fin24.

Umaarufu wa Whatasap inayomilikiwa na facebook umeongezeka nchini Afrika Kusini ukiwa na watumiaji Zaidi ya milioni kumi kwa mujibu wa ripoti ya World Wide Worx na Fuseware.

Kampuni mbili kubwa za simu Afrika kusini Vodacom na MTN mwaka uliopita zilitoa wito wa kudhibitiwa kwa huduma hizo.

Kuna hawa washiriki wanaopata manufaa makubwa katika sekta hii bila kutumia pesa. Tutapataje usawa?" afisa mmoja wa MTN alinukuliwa akisema.Kamati ya bunge kuhusu mawasiliano ya posta ilipanga kufanya kikao hicho tarehe 26 mwezi January kujadili sera za kuingilia kati swala hilo.
 Chanzo:BBC

TTCL YAKOPA DOLA MILIONI 22 KUSAMBZA MTANDAO WA 3G NA 4G LTE

http://www.thehabari.com/wp-content/uploads/2016/01/bt.jpg
Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Dk. Kamugisha Kazaura (kushoto) akibadilishana hati ya makubaliano ya mkopo na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Uwekezaji (TIB), Jaffer Machano mara baada ya kutiliana saini.

Kampuni ya Simu Tanzania TTCL na Benki ya TIB zimetiliana saini Mkataba wa makubaliano ya dhamana ya Benki na Mkopo wa Dola za Marekani Milioni 22 ikiwa ni awamu ya kwanza ya mkopo wa Dola za Marekani milioni 329 itakazopewa TTCL.

Akizungumza katika hafla ya kusaini hati ya makubaliano ya mkopo huo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Dk. Kamugisha Kazaura alisema mkopo huo ni mahususi kwa ajili ya kuiwezesha TTCL kusimika mitambo mipya na ya kisasa kuboresha huduma zake kwa kujenga na kusambaza huduma za  Mitandao ya 3G na 4G LTE  nchini kote.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TIB, Jaffer Machano amesema katika kutimiza wajibu wa TIB kama benki ya maendeleo, ujenzi wa miundombinu umepewa kipaumbele na hii ni pamoja na miundombinu ya sekta ya Mawasiliano.

Baadhi ya huduma za TTCL zitakazoimarika baada ya uwezeshaji huu ni pamoja huduma za simu na intaneti yenye kasi kubwa inayowezesha huduma za kijamii kufanyika kwa urahisi kwa njia ya mtandao.

 Huduma kama vile za Elimu kwa njia ya mtandao (E education), Afya kwa njia ya mtandao (E health) na huduma katika Sekta nyingine za kiuchumi kama vile Biashara, Viwanda na Kilimo nazo zitanufaika sana ambapo wafanyabiashara na wazalishaji wa bidhaa mbalimbali watapata Mawasiliano ya uhakika katika kufanikisha shughuli zao.

Kampuni ya Simu Tanzania TTCL ipo mbioni kuanzisha huduma ya kusafirisha fedha kwa njia ya Mtandao ifikapo robo ya pili ya mwaka huu ili kutekeleza ombi la muda mrefu la Wateja wake wanaohitaji sana kuanzishwa kwa huduma hii kutokana na Mtandao mpana wa Kampuni uliosambaa ndani na nje ya nchi na unafuu wa gharama.

Tuesday, January 12, 2016

TWITTER KUONGEZA IDADI YA HERUFI HADI 10,000

 

Twitter ina mpango wa kuongeza kiwango cha idadi ya herufi zinazoandikwa katika nafasi ya ujumbe kutoka 140 hadi 10,000 sawa na ujumbe wa kawaida.

Baada ya uvumi mtandao huo sasa umeamua kuongeza idadi hiyo.

Ni hatua ya hivi karibuni ya Twitter kuweza kuwavutia wateja zaidi.

Mkuu wa Twitter na mwanzilishi Jack Dorsey amesema kuwa ataongeza idadi ya kiwango cha herufi zitakazotumika.

Iwapo Twitter itakubali kiwango cha ujumbe wenye herufi 10,000 huenda ikazalisha ujumbe wa maneno 1,700.

Katika ujumbe wake ,Jack Dorsey ameandika kwamba Twitter tayari imebaini kwamba wengi wa wateja wake milioni 300 tayari wamekuwa wakipiga picha kubwa za ujumbe mrefu katika ujumbe wao.

Amesema kuwa Twitter inajaribu kutafuta mbinu za kuwapa watu zaidi uwezo wa kujielezea bila kuchafua huduma hiyo.
Chanzo:BBC

Tuesday, January 5, 2016

ELIMU DUNI YA MTANDAO CHANZO CHA MATUMIZI MABAYA YA MITANDAO YA KIJAMII



 

Wadau mbalimbali wa mitandao ya kijamii jijini Arusha wameeleza kuwa, Elimu duni kuhusu matumizi ya mtandao ndio chanzo cha matumizi mabaya ya mitandao hiyo hali inayosababisha migogoro katika jamii. 

Akizungumzia suala hilo Bwana Fransis Kimati ameeleza kuwa elimu duni kuhusu mitandao ikiwemo ukuaji wa sayansi na Teknolojia ndio chanzo kikubwa cha mmomonyoko wa maadili hususani kwa vijana. 

Kwa upande wake Bw. Joshua Jacob ambaye ni mwandishi wa vitabu amesema, hatua zinataikiwa kuchukuliwa ikiwemo utolewaji elimu kwa rika la vijana ambao ndio kundi kubwa la watumiji wa mitandao, kupitia vitabu, majarida warsha na matamasha mbalimbali, ili kubadilisha mitazamo mibaya kwa vijana.

Aidha wamesema kuwa dhamira ya kuwepo mitandao ya kijamii mbalimbali ikiwemo Facebook,Twiter ni nzuri lakini bado jamii haijawa na ufahamu wa kutumia mitandao hiyo kwa kujiendeleza katika njanja mbalimbali.

Thursday, December 31, 2015

USICHOFAHAMU KUHUSU WHATSAPP HIKI HAPA

 Whatsapp-1
Screen Shot 2015-12-31 at 12.25.45 PM
Maeneo yaliyopata matatizo ya WhatsApp kutofanyakazi kwa mujibu wa DownDetector
Mtandao wa kijamii wa WhatsApp ulipata mushikeli kwa muda wa masaa kadhaa jana Alhamisi Desemba 31,2015 muda mfupi kabla ya kuingia mwaka mpya hali ambayo ilisababisha watumiaji wa mtandao huo sehemu mbalimbali duniani kushindwa kutuma na kupokea ujumbe wa Kheri ya Mwaka Mpya kama ilivyotarajiwa.

Kwa mujibu wa account ya twitter inayoonesha mwenendo wa WhatsApp umeonesha kuwa tatizo la jana lilishatokea katika nyakati tofauti tofauti ambazo ni Nov 8,2011,Des 1,5,2011,Machi 11,2012,Mei 8,2012,Agosti 29,2012,Oktoba 15 2013 na Feb 22,2014.

Kwa mujibu wa tovuti ya DownDetector, ambayo hujihusisha na kufuatilia matatizo yanayotokea kwenye mitandao imelezwa kuwa tatizo hilo lilionekana hasa katika nchi za Uingereza na Ujerumani huku ikielezwa kuwa tatizo hilo halikuwa kubwa nchini Marekani.

Jumla ya watu milioni 900 duniani wamejiunga na mtandao huo ambao unatumika katika simu za mikononi zenye mifumo endeshi ya iOS na Android huku kukiwa na utumaji wa ujumbe bilioni 10 kila siku.




SERIKALI YAPIGA MARUFUKU MATUMIZI YA BARUA PEPE ZA KAWAIDA KATIKA MAWASILIANO YAKE



Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki (kushoto) akipokelewa na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao Dkt. Bakari Jabiri leo alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala hiyo jijini Dar es salaam. 
Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki (katikati) akiwasili Ofisi za Wakala ya Serikali Mtandao kwa ziara ya kikazi leo jijini Dar es salaam.
Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki (kulia) akitembelea maeneo mbalimbali ya Ofisi za Wakala ya Serikali Mtandao leo. Kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao Dkt. Bakari Jabiri leo alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala hiyo jijini Dar es salaam. 
Mkurugenzi wa Uratibu wa Miundombinu ya TEHAMA wa Wakala ya Serikali Mtandao Bw. Benjamin Dotto akitoa ufafanuzi kwa Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki (kulia) kuhusu kituo cha ufuatiliaji mifumo ya mawasiliano Serikalini leo jijini Dar es salaam. 



Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki akizungumza na Watendaji na baadhi ya Wafanyakazi wa Wakala ya Serikali Mtandao leo alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala hiyo jijini Dar es salaam. 
 
Serikali imepiga marufuku matumizi ya Barua pepe za kawaida kwa watumishi wa umma wanaotuma au kupokea taarifa za Serikali na kuwataka watumishi hao kuhakikisha kuwa wanatumia mfumo rasmi wa Mawasiliano ya Barua Pepe Serikalini (GMS) ulioanzishwa na Serikali kwa lengo la kuimarisha mawasiliano kwa njia ya Mtandao. 

  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.Angella Kairuki ametoa agizo hilo alipokuwa akizungumza na Watendaji na Watumishi wa Wakala ya Serikali Mtandao ( e Government Agency) wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji na ufanisi wa matumizi ya TEHAMA Serikalini. 

  Ameeleza kuwa kuna watumishi 7000 wanaotumia anwani za Barua pepe za Serikali ,idadi ambayo ni ndogo lazima iongezeke, hivyo serikali haiwezi kuendelea kuruhusu utumaji wa taarifa za Serikali kwa kutumia Barua Pepe nje ya mfumo huo huku akifafanua kuwa Serikali haijakataza matumizi ya barua pepe za kawaida kwenye mawasiliano binafsi. 

Amesema kwa kutambua umuhimu wa uimarishaji wa mawasiliano ya TEKINOHAMA Serikalini na kuongezeka kwa matumizi ya TEKINOHAMA katika utumaji wa taarifa kupitia mitandao mbalimbali ipo haja ya kuweka msisitizo kwa watumishi wa umma kutumia Barua Pepe za Serikali. 

Mhe. Kairuki amewataka watendaji wa Wakala hiyo kuhakikisha kuwa wanasimamia uratibu wa zoezi hilo ili kuhakikisha kuwa Wizara, Idara na Taasisi zote za umma zinaunganishwa na mfumo rasmi wa Serikali ili kuwa na mfumo mmoja wa Mawasiliano huku akitoa siku 60 kukamilika kwa zoezi hilo katika taasisi zingine.


Thursday, December 24, 2015

TTCL YAZINDUA TEKNOLOJIA YA 4G LTE

 Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Simu nchini Tanzania (TTCL), Dk. Kamugisha Kazaura (kushoto) na Ofisa Ufundi (IT) wa kampuni hiyo, Rehema Maswanya (kulia) kwa pamoja wakifungua pazia kuashiria uzinduzi wa teknolojia ya 4G LTE iliyozinduliwa leo jijini Dar es Salaam.

 
Kampuni ya Simu nchini Tanzania (TTCL) imezinduwa mtandao unaotumia teknolojia ya 4G LTE unaoanza kutoa huduma jijini Dar es Salaam. Mtandao huo wenye teknolojia mpya na ya kisasa wenye kasi kubwa utatoa huduma katika maeneo 11 ambayo ni pamoja na Uwanja wa Ndege wa Mwalimu J.K. Nyerere, Pugu Road, Posta Mpya, Upanga, Kinondoni, Ubungo, Oysterbay, Mwenge, Mbezi Tangibovu, Mbezi Exchange, Kunduchi Salasala, na Wazi Tegeta.

Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati akizinduwa rasmi teknolojia hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Dk. Kamugisha Kazaura alisema licha ya kuzinduwa huduma hiyo katika maeneo 11 kwa sasa mafundi wa kampuni hiyo wapo kazini wakiendelea na awamu ya pili ya kufunga mitambo ili huduma hiyo itolewe pia katika maeneo mengine 14 ya jiji la Dar es Salaam.

Aliyataja maeneo mengine ambayo mitambo inaendelea kufungwa kwa sasa kuwa ni pamoja na Kigamboni, Masaki, Temeke, Kimara, Jangwani, Kariakoo, Chuo Kikuu, Kurasini, Mbezi Chini Gongo la Mboto, Tabata, Kibamba, Kongowe na Bunju.

Tuesday, December 8, 2015

POLISI ARUSHA KUTUMIA WHATSAPP KUDHIBITI UHALIFU


 Image result for whatsapp

Jeshi la Polisi mkoani Arusha na Kampuni za Ulinzi wameweka mkakati wa kushirikiana katika kupeana taarifa za uhalifu kwa kutumia mtandao wa kijamii wa WhatsApp.

Mpango huo umetangazwa na Mkuu wa Operation wa Jeshi la Polisi Arusha Edward Balele ambapo amesema awali taarifa zilikuwa zikiwafikia walengwa kwa mtindo wa ujumbe mfupi (SMS) lakini kwa kutumia mfumo wa kikundi cha WhatsApp ambacho kitapewa jina maalum,taasisi hizo zitakuwa zinapata na kutoa taarifa kwa pamoja ambapo kila mhusika atakuwa anachingia mawazo yake huku wanawachama wengine wa kikundi hicho wakiona maoni ama ushauri wa kila mchangiaji.


JWTZ YATOA ONYO KWA WANAOPIGA PICHA NA KUZISAMBAZA KWENYE MITADAO YA KIJAMII


Mkurugenzi wa Habari  na Uhusiano  wa Jeshi la
Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa JWTZ-Kanali Ngemela Lubingo (Chanzo:Mwananchi)

Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limetoa onyo kwa wananchi kutojihusisha na upigaji picha wa vifaa vya kijeshi na kuvisambaza katika mitandao ya kijamii.

Hatua hiyo inakuja kutokana na tukio la  Desemba 3,saa 1:15 jioni ambapo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius JK Nyerere jijini Dar es salaam wafanyakazi wa Shirika la kupokea mizigo la Swiss Port wakishirikiana na wale wa shirika la Ndege la Uholanzi (KLM) kupiga picha vifaa vya kijeshi na kuvisambaza katika mitandao ya kijamii

Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa JWTZ Kanali Ngemela Lubingo amewaambia Waandishi wa Habari jijini Dar es salaamu kuwa jeshi hilo limesikitishwa na  tukio hilo la watu kujichukulia maamuzi ya kupiga picha kitu ambacho hakikuwahusu na kusambaza picha kwenye mitandao ya kijamii na kusababisha kujitokeza kwa maoni ya kupotosha jamii


Friday, December 4, 2015

WAHALIFU MTANDAO WATIKISA ANGA YA WANAUSALAMA MITANDAO

Wakati bado mafanikio mbali mbali yakijadiliwa wahalifu mtandao wamegundulika kuja na uhalifu unaotafsiriwa kuwa ni wa kihistoria na uliofanyika kwa ubunifu na umahiri wa hali ya juu ambapo wahalifu mtandao wamefanikiwa kusambaza kirusi aina ya ModPOS kinacho athiri mashine zinazotumika kukamilisha miamala wakati wa manunuzi.
 
Kirusi cha ModPOS, kimegundulika Nchini Marekani wakati wa sherehe za “Thanks Giving” ambapo watu wengi hufanya manunuzi. Kirusi hicho Kimekua kikifanikisha upotevu mkubwa wa pesa wakati wa miamala.

Mara baada ya ugunduzi huo wa ModPOS, mijadala kupitia mtandao ilianza baina ya wanausalama mitandao ili kuweza kufanikisha mambo makubwa matatu. Moja ni kuweza kugundua chanzo na jinsi ilivyo fanikishwa kuwepo bila kugundulika (Inaaminika kimedumu muda – Taarifa ambazo bado zinafatiliwa) Pili, Ilikua ni kutafuta suluhu ya kirusi hicho ili kiweze kuondolewa na Tatu, ni kupanga namna ya kukuza uelewa wa namna ya kujikinga na janga hili la ModPOS.

Hadi sasa bado hapajapatikana suluhu na inahofiwa huwenda kutokana na sherehe za mwisho wa mwaka kirusi hicho kusambaa maeneo mengine huku mataifa yakitakiwa kuchukua tahadhari. Inakadiriwa kama kitaendelea kutopatiwa suluhu; pesa nyingi zitaishia mikononi mwa wahalifu mtandao na hasara itakayopatikana ni kubwa zaidi kupata kutokea.

Wakati hayo yakiendelea kuwa ni mjadala wa vuta nikuvute. Wahalifu wakadukua Kampuni ya VTech inayotengeneza midoli ya watoto ya kielektroniki kutumia TEKINOHAMA ambapo walifanikiwa kuiba taarifa zaidi ya milioni tano ikiwa ni pamoja na Picha za watoto, Mawasilianao ya watoto na wazazi wao, Sauti za watoto, na taarifa za miamala wakati wa manunuzi.

Inaaminika kutokana na umakini mkubwa wanausalama mtandao wamekua wakiweka juu ya kuwalinda watoto wawapo mtandaoni kitu ambacho kimepelekea kua na program ya kidunia maarufu kama “Child Online Protection – COP” yenye dhamira ya kuhakiki watoto wanabaki salama watumiapo TEKINOHAMA/ Mitandao, Wahalifu walitumia udukuzi wa VTech ili kuhamisha mawazo ya kukabiliana na ModPOS na badala yake nguvu kubwa ihamie kwenye udukuzi VTech.

Kufuatia udukuzi huo kwenye kampuni ya VTech wanausalama mtandao walishauri Kampuni hiyo kusitisha huduma zake za mtandao mara moja na kuendelea kutafuta suluhu ya tatizo. Huku kampuni hiyo ikitakiwa kuhakiki taarifa zilizo dukuliwa hazipatikani/ kusambwazwa mitandaoni. Kampuni ya VTech tayari imechukua uamuzi wa kusitisha huduma zake mtandao.

Hayo yakijiri, Nchini Kenya nako wameshatoa Ripoti/taarifa za mwaka kuhusiana na uhalifu mtandao ambapo uhalifu mtandao umeonekana kukua zaidi. Taarifa ilifafanua uhaifu mtando umebadili taswira na kuwa si tu wa kudukua maneno ya siri bali ni taarifa zinazoweza kupelekea mabilioni ya dola kuishia kwa wahalifu mtandao. Jitihada za dhati zimeendelea nchini Kenya ili kukabiliana na uhalifu huu mtandao.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Tanzania nayo haijabaki salama, Baada ya uhalifu mtandao maarufu kwajina la “vikoba” ulioshika kasi kipindi kifupi cha nyuma uliosababisha waathirika kuibiwa fedha zao na wahalifu mtandao. Baadae elimu juu ya uhalifu huo ilisambaa na hatimae kupungua sasa wahalifu mtandao wamekuja na aina mpya ya uhalifu mtandao wenye dhamira ya kuiba taarifa za watu baada ya kufanikiwa kutengeneza program yenye kuwashawishi watu kuingiza taarifa za wengine kwa madhumuni ya kudukua taarifa za watu binafsi.Ikumbukwe hili ni kosa na lazima wananchi wawe makini kwenye hili.

Aidha, wahalifu matandao wajakomea hapo, Kwa mujibu wa taarifa ya kampuni ya kiusalama mtandao ya “Symantec” imefanikiwa kugundua mbinu ambayo wahalifu mtandao wamekua wakitumia mtandao wa kijamii wa “LinkedIn” ambapo wahalifu wamekua waki dhamiria zaidi kuiba taarifa zinazopatikana kwenye mtandao huo baada ya kuweka ukaribu na watumiaji mtandao huo kwa kuwaomba urafiki na baadae kutumia taarifa zilizopo huko kufanya udukuzi.

Hili tayari Symantec kwa kushirikiana na LinkedIn imeanza opareheni funga akounti zozote zinazobainika kuwa ni za wahalifu mtandao na tunategemea kupata taarifa yake kamili hapo baadae.

Matukio hayo na mengine yanayowea kujitokeza watai tunaelekea mwisho wa mwaka ushauri mkubwa umeendelea kutolewa ku kuhakiki panakua na mpango endelevu wa kukuza uelewa wa matumizi salama ya mitandao (Cybersecurity awareness).

Pamoja na hilo mataifa yana aswa kua na tabia ya kuhakiki yanatambua kwa ukaribu sana viashiria vyovyote vya kihalifu mtandao ili kuweza kuweka mataifa yao salama kimtandao. Zaidi ni pamoja na kukuza nguvu kazi watu kwenye sekta ya usalama mtandao pamoja  na kua na matumizi ya watu sahihi katika kukabiliana na uhalifu mtandao.


Natoa wito wa kutambua uhalifu mtandao upo na una madhara makubwa katika sekta zote kuanzia Kiuchumi, Kijamii, Kisiasa, nakadhaika endapo hatua kuanzia ngazi ya mtu binafsi hazitachukuliwa ili kuhakiki pana patikana usalama katika mitandao. Tujenge tabia yay a kutafakari kabla ya kutumia mitandao ili kuhakiki hatusababishi madhara kwa kuanzia kwa mtu binafsi pamoja na kwa wengine.

Na:Yusuph Kileo

Popular Posts

Labels