Saturday, November 22, 2014

WAHALIFU MTANDAO WATEGEMEWA KUELEKEZA NGUVU ZAO BARANI AFRIKA

Mtaalamu wa masuala ya usalama kwenye Mtandao Yusuph Kileo akiwasilisha mada
Itakumbukwa katika mkutano uliofanyika  mapema mwezi huu  jijini "CAIRO" hofu ya ukuwaji wa uhalifu mtandao unaoweza kurudisha nyuma uchumi wa mataifa ya Afrika  ulipata kujadiliwa kwa kina huku nchi ya Misri ikionyesha washiriki wa mkutano huo jitihada inayoendelea nayo katika kukabiliana na uhalifu mtandao.

Imeripotiwa na Mtandao wa "MGAFRICA" kuhusiana na kilichojiri katika mkutano uliokamilika jijini Johannesburg, Afrika kusini wa maswala ya usalama mitandao ambapo Bara la Afrika limetabiriwa kuwa na ukuaji wa uhalifu mtandao kutokana na mikakati dhaifu ya kujiweka salama huku ikiwapatia wahalifu mtandao urahisi mkubwa wa kuleta maafa siku za usoni.

 
Kumeendelea kuwa na wimbi kubwa la uhalifu mitandao ingawa jitihada za kukabiliana na uhalifu huo zimeendelea  kugharimu mataifa mengi hivi sasa. Mataifa yamekua yakiwekeza kwenye maswala ya usalama mitandao lakini bado wahalifu mtandao wameonekana kuendelea kutamba.

Mkutano huo wa maswala ya  usalama mitandao uliangazia kwa karibu  sababu za ukuaji wa uhalifu mtandao na nini kifanyike kwa mataifa ili kuweza kupiga hatua ya kubaki salama kimtandao. Wataalam wa maswala Mtandao kutoka katika mataifa mbali mbali walikutana  kuyajadili mambo hayo yafuatayo:-

Swala la kukuza uwelewa kwa watumiaji mtandao kuhusu matumizi salama ya mitandao lilionekana bado ni changamoto katika mataifa mengi. Na njia rafiki za kuhakiki kampeni hii ya kuhamasisha umma juu ya matumizi salama ilipelekea mambo mengi kuangaziwa macho huku "TOVUTI" maalum kwa ajili ya uelewa wa matumizi salama mitandao ikipata kuzinduliwa.

Sheria nazo zilionekana kuwa changamoto kubwa sana barani Afrika. Kumekua na kusua sua sana kwa sheria mitandao kuanza kufanyiwa kazi huku Wataalam kutoka katika vyombo vya sheria (Mahakama) wakionyesha hali wanayokumbana nayo katika kutolea maamuzi dhidi ya uhalifu mtandao.

Tulipata kufafanua na kueleza usalama mitandao haunabudi kwenda sambamba na sheria zake maalum zinazopaswa kupitiwa mara kwa mara na kuborehwa ili kuendana na wakati. Bila kufanya hivyo hali ya wahalifu mtandao kufanya matukio na kutopatiwa adhabu stahiki itaendelea kuchangia ukuaji wa uhalifu huu.

Swala la Uhaba wa wataalam nalo halikubaki nyuma. Mjadala mkubwa uliangazia jitihada mbali mbali za mataifa zinazofanywa ili kuweza kuwa na wataalam wakutosha wenye uwezo sahihi wa kujua namna ya kudhibiti, kukabiliana na kuzuia uhalifu mtandao.

Ushirikiano katika maswala ya usalama mitandao kuanzia ngazi ya kitaifa kibara na kimataifa ilionekana bado ni changamoto kubwa sana ambayo bado ku safari ndefu kuhakiki tunafikia malengo. Njia rafiki ya kuhakiki tunakua na utamaduni wa kushirikiana kuanzia ngazi ya taifa moja moja kabla ya kuvuka mipaka ilisisitizwa kufanyiwa kazi ili kurahisisha vita dhidi ya uhalifu mtandao.

Wataalam mbali mbali walipata fursa ya kuonyesha kwa vitendo gunduzi mpya za kisasa zenye kurahisisha uwezo wa kubaini, kuzuia na kukabiliana na uhalifu mtandao ambapo kila gunduzi ilipata kujadiliwa kwa kina ili kuweza kuleta tija dhidi ya mapambano na uhalifu mtandao.

Mataifa na vikundi mbali mbali pia vilipata fursa ya kuonyesha takwimu mbali mbali za maswala ya uhalifu mtandao na njia mbazo mataifa hayo yameendelea kukabiliana na wimbi kubwa la wahalifu mtandao. Mjadala mkubwa katika kuzikosoa na kurekebisha jitihada hizo ulipata kuonekana wenye malengo madhubuti ya kuwa na bara salama kimtandao.


Paliangaziwa pia vifaa mbali mbali vya kiusalama mitandao ambapo vimeendelea kutumika ipasavyo kuhakiki uhalifu mtandao unakabiliwa ipasavyo. Huku pakitolewa baadhi ya vifaa hivyo kwa washiriki ili kuweza kuongeza tija kwenye mapambano dhidi ya uhalifu mtandao katika mataifa mbalimbali barani Afrika.
Na Yusuph Kileo

SERIKALI YA TANZANIA YATAKIWA KUIMARISHA KITENGO CHA KUKABILIANA NA WAHALIFU KUPITIA MITANDAO



Serikali nchini Tanzania  imetakiwa kuimarisha kitengo cha upelelezi na ufatiliaji wa makosa jinai yanayofanywa kupitia mitandao ya simu za mkononi na intaneti.

Rai hiyo imetolewa na wamiliki, wafanya kazi  na mawakala  wa makampuni ya kutuma na kusafirisha fedha  jijini mwanza yaani tigo pesa, M pesa, airtel money,  na mashirika  mengine ambapo wameiomba serikali kuunda  kamati ya upelelezi na wataalamu wa  kuchunguza mienendo ya watu wanao tumia simu za mkononi na intaneti kutapeli wananchi mamillioni ya pesa.

Mmoja kati ya wafanyakazi wa makampuni hayo Iyuko Kiyumba amesema kuwa  vituo vingi vya polisi jijini Mwanza havina  wapelelezi wala  wajuzi wanao weza kufuatilia  ipasavyo wezi wanao tumia njia za mitando  hivyo watuhumiwa wanapo kamatwa huachwa huru baada  ya kutoa ushahidi na mahakama kukosa nguvu ya kuwatia hatiani watu hawa. 

Taarifa zilizotolewa na wamiliki wa makampuni hayo zimedai kuwa baadhi ya wezi  wamesajili laini hizo kwa majina ya viongozi wa serikali  ambapo huzitumia kuwaibia maafisa wakubwa wa ngazi za juu na wananchi mbalimbali kwa kutumia njia za kimtandao.


Wednesday, November 19, 2014

MSWADA WA KUZUIA UKUSANYAJI WA DATA ZA SIMU MAREKANI WAZUIWA NA WABUNGE



Mswada  ambao  ungezuia  ukusanyaji  wa  data  za  simu unaofanywa  na  shirika  la  usalama  wa  taifa  nchini  Marekani , NSA, umezuiwa  na  wabunge  mjini  Washington.  

Kura  hiyo  katika baraza  la  Seneti  ilikuwa  kura  58  za  ndio  na 42  za  hapana , ikiwa  ni  kura  mbili chini  ya  kura  60  zinazohitajiwa  kuupitisha mswada  huo.

Mswada  huo uliokataliwa  ungefikisha  mwisho  ukusanyaji  wa  data za  simu  za  mamilioni  ya  Wamarekani.   

Wanaoupinga  wanasema ukusanyaji  wa  data  ni  muhimu  kwa  ajili  ya  juhudi  za  kupambana na  ugaidi.

Kiwango  cha  udukuzi  huo ulikuwa  miongoni  mwa  ufichuaji uliofanywa  na  mfanyakazi  wa  zamani  wa  shirika  la  NSA Edward Snowden.

SITA WAKAMATWA KWA TUHUMA ZA UTAPELI KWA NJIA YA MTANDAO WA SIMU



Watu sita wanaosadikiwa kuwa ni matapeli kwa njia ya mtandao wa simu wamekamatwa jijini mwanza baada ya kufanya utapeli kwa watu mbali  mbali kwa njia ya simu huku wakitumia majina ya watu maarufu jijini humo.

Akizungumza na waandishi wa habari kamanda wa polisi jijini Mwanza Valentino Mlohola amesema kuwa, November 5 mwaka huu kijana mmoja anayejulikana kwa jina la Eradius Christian alisajili namba ya simu kwa jina linalofanana na jina la kamanda huyo.

Kamanda huyo amesema kuwa watu hao wamekuwa wakisajili majina yanayofanana na viongozi mbali mbali wa serikali na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwa njia ya simu kitu ambacho ni kosa kisheria na watu hao wamefikishwa kituo cha polisi na upelelezi ukikamilika watafikishwa mahakamani.

Mlohola amesema, kipindi hiki cha kuelekea katika sikukuu za mwisho wa mwaka wananchi wanapaswa kuwa makini kwani matapeli watakuwa wengi katika kutafuta fedha za sikukuuna na amewaomba wananchi wakihisi wizi wa namna hiyo watoe taarifa polisi.

Thursday, November 13, 2014

UNESCO NA SAMSUNG KUJENGA KIJIJI CHA DIGITALI OLOLOSOKWAN


DSC_0062
Mwakilishi mkazi shirika la UNESCO nchini Bi. Zulmira Rodrigues  na Mkurugenzi wa  Samsung Electronics nchini Tanzania, Bw. Mike Seo wakibadilishana nyaraka za makubaliano hayo yaliyofanyika ofisi za UNESCO.(Picha na Philemon Solomon).
Na Mwandishi wetu
Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni  (UNESCO) limetiliana saini mkataba na kampuni ya elektroniki ya Samsung ya ujenzi wa kijiji cha digitali cha Ololosokwan, Loliondo.

 Makubaliano hayo yalitiwa saini hivi karibuni kati ya Mwakilishi mkazi Unesco nchini Bi. Zulmira Rodrigues  na Mkurugenzi wa  Samsung Electronics nchini Tanzania, Bw. Mike Seo katika hafla iliyofanyika ofisi za UNESCO.

Kijiji hicho kitakuwa na  shule yenye Teknohama ikiwa na maunganisho ya intaneti, kiliniki ya kisasa ikiwa na kituo cha  teknolojia ya mawasiliano yenye kuwezesha utabibu (telemedicine) na  jenereta linalotumia nguvu za jua kwa ajili ya kijiji hicho.

Utiaji saini huo ulioshuhudiwa na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, bi. Leah Kihimbi kutoka wizara ya habari, vijana, utamaduni na michezo na Dkt. N.  Iriya kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Dar es Salaam na wafanyakazi wa UNESCO.

Katika hafla hiyo Bi. Rodrigues  amesema kwamba mradi huo utawezesha UNESCO kuwapatia vijana wa Kimasai elimu kutokana na ukweli kuwa kwa utamaduni na kazi zao za ufugaji wamekuwa wakipata shida ya kupata elimu.
DSC_0002
Baadhi ya wafanyakazi wa UNESCO na Samsung wakifuatilia kwa umakini hafla hiyo fupi ya kutiliana saini makubaliano baina ya Samsung Tanzania na UNESCO.
“Kupitia kijiji hiki vijana wataendelea na masomo hata kama wanachunga mifugo yao”, alisema Bi. Rodrigues.

Naye  Mkurugenzi wa Samsung Electronics nchini Tanzania miongoni mwa manufaa makubwa yatakayopatikana katika mradi huo wa kijiji cha digitali huko Loliondo  ni kuweza kupata nishati  rahisi na iliyo rafiki kwa mazingira.

Alisema kwamba Afrika imekuwa mstari wa mbele katika uanzishaji wa vijiji vya digitali. Aidha kwa kitendo hicho Afrika inaonesha dunia ni kwa namna teknolojia inaweza kutumika kuleta mabadikliko chanya  yanayotakiwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi waliopo vijijini.

Bi Leah Kihimbi ambaye alimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya habari,vijana, utamaduni na michezo, alisema kupitia vijiji vya digitali  itawezekana kutekeleza program ya elimu  kwa watu wanaoishi Loliondo huku tamaduni zao zikihifadhiwa.

Kijiji hicho cha Loliondo kitakuwa cha nne katika vijiji vya kidigitali barani Afrika. Inatarajiwa kwamba kijiji kingine kitajengwa mjini Zanzibar kwa ushirikiano wa UNESCO na Samsung Electronics mwaka 2015.
Untitled 1
Pichani ni muonekano wa mchoro wa kijiji hicho utakavyokua.

Tuesday, November 11, 2014

WAMILIKI WA BLOG TANZANIA WATAKIWA KUFUATA MAADILI YA UANDISHI WA HABARI




Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo nchini Tanzania Assah Mwambene

Mhandisi wa TCRA,Andrew Kisaka akiwasilisha Mada kuhusu maadili ya Uandishi  na Utangazaji  wa Habari

Wamiliki wa blog mbalimbali waliohudhuria katika mkutano huo


Kamati ya muda ya wamiliki wa blog iliyochaguliwa leo

Mwenyekiti wa Kamati ya wamiliki wa blog Joachim Mushi
Serikali imewataka wamiliki na waandishi wa blog nchini kuzingatia maadili ya taaluma ya uandishi wa habari wakati wa mchakato wa kuelekea kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mwezi ujao na uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani.

Akizungumza jijini Dar es salaam hii leo wakati wa ufungaji wa mkutano wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Wamiliki wa blog mbalimbali nchini Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Tanzania Assah Mwambene amesema serikali inatambua blog zinafanya kazi ya kutoa habari sawa na vyombo vingine vya habari lakini vinapaswa kuzingatia uandishi wa mambo ya msingi kwa kufuata maadili ya uandishi wa habari.

Mwambene ambaye pia ni Msemaji wa serikali ameeleza kuwa lazima wamiliki na waandishi wa blog wajue wamechukua wajibu mkubwa unaoendana na wajibu wa kuwajibika kwa wananchi wanaowandikia habari wa kuzingatia maadili.


Awali akizungumza kwenye mkutano huo Mkurugenzi wa Utangazaji wa TCRA Habbi Gunze amesema waandishi na wamiliki wa blog wananafasi ya kusaidia umma kuweza kuelewa masuala mbalimbali ya uchaguzi pasipo upendeleo wowote wala uchochezi.


Kumekua na malalamiko toka kwa  wananchi kutokana na habari mbalimbali zinazoandikwa kwenye baadhi ya blog kwa kutozingatia maadili ya uandishi wa habari na utamaduni wa mtanzania jambo ambalo ni changamoto kwa serikali kutokana na uhuru uliopo kwa wamiliki wa blogi hizo na ukosefu wa sheria zinazowaongoza.

Popular Posts

Labels